Select Page

Masomo ya Misa Feb 26

Tumsifu Yesu Kristu… Karibu Katika Masomo ya Misa 26/02/2024

2024 FEBRUARI 26 JUMATATU: JUMA 2 LA KWARESIMA
Mt. Alexander wa Alexandria 
Urujuani
Zaburi: Juma 2

Somo 1. Dan 9: 4-10

Ee Bwana, Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika amri zake; tumefanya dhambi, tumefanya ukaidi, tumetenda maovu, tumeasi, naam, hata kwa kuyaacha maagizo yako na hukumu zako; wala hatukuwasikiliza watumishi wako, manabii, ambao kwa jina lako walisema na wafalme wetu, na wakuu wetu, na baba zetu, na watu wote wa nchi. Ee Bwana, haki ina wewe lakini kwetu sisi kuna haya ya uso, kama hivi leo; kwa watu wa Yuda, na kwa wenyeji wa Yerusalemu, na kwa Israeli wote, walio karibu na hao walio mbali, katika nchi zote ulikowafukuza, kwa sababu ya makosa yao waliyokukosa. Ee Bwana, kwetu sisi kuna haya ya uso, kwa wafalme wetu, na wakuu wetu, na baba zetu, kwa sababu tumekutenda dhambi. Rehema na msamaha ni kwa Bwana Mungu wetu, ingawa tumemwasi; wala hatukuitii sauti ya Bwana, Mungu wetu, kwa kwenda katika sheria zake, alizoziweka mbele yetu kwa kinywa cha watumishi wake, manabii.

Wimbo wa Katikati. Zab 79:8, 9-11

1. Usikumbuke juu yetu maovu ya baba zetu,
Rehema zako zije kutulaki hima,
Kwa maana tumeadhilika sana. (K)

(K) Usitutende sawasawa na hatia zetu, Ee Bwana.
 
2. Ee Mungu wokovu wetu utusaidie.
Kwa ajili ya utukufu wa jina lako.
Utuokoe, utughofiri dhambi zetu,
Kwa ajili ya jina lako. (K)  

3. Kuugua kwake aliyefungwa na kuingie mbele zako.
Kwa kadiri ya ya uweza wa mkono wako
Uwahifadhi wana wa mauti.
Na sisi tulio watu wako, na kondoo za malisho yako,
Tutakushukuru milele;
Tutazisimulia sifa zako kizazi kwa kizazi. (K)

Injili. Lk 6:36-38

Yesu aliwaambia wafuasi wake: ”Iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma. Msihukumu, nanyi hamtahukumiwa; msilaumu, nanyi hamtalaumiwa; achilieni, nanyi mtaachiliwa. Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwasukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa”.

TAFAKARI

MWENYE KUTUSTAHILISHA NI MUNGU: Ni yapi mastahili yetu mbele ya Mungu? Swali hili ni la msingi katika maisha yetu. Katika kutafuta majibu ya swali hili tutajikuta kuwa hatuna mastahili kwani sisi tu wadhambi. Pamoja na dhana hii wanadamu tumeendelea kushutumiana, kuuana, kulaumiana na hata kukosa huruma kwa wenzetu. Namna hii ya kutostahili mbele ya Mungu inaleta msukumo kwa Yesu kutukumbusha kuwa na huruma. Yesu alieleza kuwa kipimo tukitumiacho ndicho kitakachotumika kwetu pia. Nabii Danieli anaeleza wazi kuwa tumemwasi Mungu kwa kuwa hatukuitii sauti yake aliyotupatia kwa njia ya watu wake. Nabii Danieli anakiri kuwa tumetenda dhambi. Kukosa huruma kwa wenzetu, kuwahukumu wenzetu pasi mastahili ni dhambi. Wapendwa, ili tuweze kuoneana huruma ni lazima tujifunze kuonja maumivu ya watu wale tunaowatendea vibaya. Tunapokosa huruma tunazalisha chuki, ugomvi, mauaji n.k. Tufuate mfano wa nabii Danieli, tutambue makosa yetu, tujiulize kwanini hatujawahurumia wenzetu na tuwe tayari kujirekebisha.

SALA: Ee Bwana, utujalie mapendo na huruma kwa wote. amina.

Masomo ya Misa Feb 25

Tumsifu Yesu Kristu… Karibu Katika Masomo ya Misa Takatifu 25/02/2024

2024 FEBRUARI 24: DOMINIKA YA 2 YA KWARESIMA
Urujuani
Zaburi: Juma 2

Somo 1. Mwa 22 :1-2, 9a, 10-13, 15-18

Mungu alimjaribu Ibrahimu, akamwambia, Ee Ibrahimu! Naye akasema, Mimi hapa. Akasema, Umchukue mwanao, mwana wako wa pekee, umpendaye, Isaka, ukaende zako mpaka nchi ya Moria, ukamtoe sadaka ya kuteketezwa huko juu ya mlima mmojawapo nitakaokuambia. Wakafika mahali pale alipoambiwa na Mungu, Ibrahimu akanyosha mkono wake, akakitwaa kisu ili amchinje mwanawe. Ndipo malaika wa Bwana akamwita kutoka mbinguni, akasema, Ibrahimu! Ibrahimu! Naye akasema, Mimi hapa. Akasema, Usimnyoshee kijana mkono wako, wala usimtendee neno; kwa maana sasa ninajua ya kuwa unamcha Mungu, iwapo hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee. Ibrahimu akainua macho yake, akaangalia, na tazama, kondoo mume yuko nyuma yake, amenaswa pembe zake katika kichaka. Basi Ibrahimu akaenda akamtwaa huyo kondoo, akamtoa awe sadaka ya kuteketeza badala ya mwanawe. Malaika wa Bwana akamwita Ibrahimu mara ya pili kutoka mbinguni, akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema Bwana, kwa kuwa umetenda neno  hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee, katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama mchanga uliopo pwani; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.

Wimbo wa Katikati. Zab 116: 10,15-19 

1. Naliamini, kwa maana nitasema,
Mimi niliteswa sana.
Ina thamani machoni pa Bwana
Mauti ya wacha Mungu wake.  (K)

(K)  Nitaenenda mbele za Bwana  Katika nchi za walio hai. 

2. Ee Bwana, hakika mimi ni mtumishi wako,
Mtumishi wako, mwana na mjakazi wako,
Umevifungua vifungo vyangu.
Nitakutolea dhabihu ya kushukuru;
Na kulitangaza jina la Bwana. (K)

3. Nitaziondoa nadhiri zangu kwa Bwana,
Naam, mbele ya watu wake wote.
Katika nyua za nyumba ya Bwana,
Ndani yako, Ee Yerusalemu. (K)

Somo 2. Rum 8 :31b-34

Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu? Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajii yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye? Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.

Injili. Mk 9 :2-10

Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohane, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani, peke yao; akageuka sura yake mbele yao; mavazi yake yakimeta-meta, meupe mno, jinsi asivyoweza dobi duniani kuyafanya meupe. Wakatokewa na Eliya pamoja na Musa, nao walikua wakizungumza na Yesu. Petro akajibu, akamwambia Yesu, Rabi, ni vizuri sisi kuwapo hapa; na tufanye vibanda vitatu, kimoja chako wewe, kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya. Maana, hakujua la kunena, kwa kuwa waliingiwa na hofu nyingi. Kisha likatokea wingu, likawatia uvuli; sauti ikatoka katika lile wingu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, msikieni yeye. Mara hiyo walipotazama huku na huku, hawakuona mtu pamoja nao ila Yesu peke yake. Na walipokuwa wakishuka mlimani aliwakataza wasimweleze mtu waliyoyaona, hata Mwana wa Adamu atakapokuwa amefufuka katika wafu.

TAFAKARI

Ni Dominika ya pili ya Kwaresima. Wazo kuu ni “Kusikiliza na Kutii.” Wazo hili linapatikana katika somo la kwanza na lile la Injili. Katika somo la kwanza (Mwa 22:1-2, 9a, 10-13, 15-18), tunasikia kisa cha Ibrahimu akiombwa na Mungu amtoe sadaka mtoto wake pekee, Isaka. Ibrahimu anaambiwa: “Umchukue mwanao, mwana wako wa pekee, umpendaye, Isaka, ukaende zako mpaka nchi ya Moria, ukamtoe sadaka ya kutekezwa huko juu ya mlima mmojawapo nitakaokuambia”(Mwa 22:2). Ibrahimu akaisikiliza sauti hii ya Mungu, akamtii. Hivyo akamchukua Isaka hadi mlimani. Na mara walipofika pale Ibrahimu akanyosha mkono wake, akakitwaa kisu ili amchinje mwanawe. Kitendo hiki cha Ibrahimu kumsikiliza Mungu na kuitii sauti yake kilimpelekea Mungu kumpatia Ibrahimu kondoo kama mbadala wa Isaka. “Ibrahimu! Ibrahimu! Usimnyonyeshee kijana wako mkono wako, wala usimtendee neno; kwa maana sasa najua kwamba unamcha Mungu, iwapo hukunizuilia nwanao, mwanao wa pekee.”(Mwa 22:12). Na mara Ibrahimu akageuka nyuma akaona kondoo mume. “Akamtwaa huyo kondoo, akamtoa awe sadaka ya kuteketeza badala ya mwanawe”(Mwa 22:13).
Simulizi hii ya Ibrahimu inatupatia maswali mawili matatu. Moja, imewezekanaje Mungu kumpa Ibrahimu ombi gumu kiasi kile? Ikumbukwe kwamba Isaka alikuwa mwana wa ahadi ya Mungu kwa Ibrahimu na Sara. Hivyo kumwomba Ibrahimu amtolee sadaka Isaka lilikuwa ni jambo ambalo kibinadamu lilikuwa gumu kulitekeleza. Pili, imewezekanaje Ibrahimu akakubali ombi la Mungu pasipo kuuliza lolote? Ikumbukwe kwamba Isaka kwa Ibrahimu ndiye alikuwa mrithi wa ile ahadi ya Mungu aliyompatia Ibrahimu wakati akimwita atoke katika nchi yake (Mwa 12:1-3). Hivyo kumtoa Isaka sadaka ni kutotimia kwa ahadi zile. Tatu, imewezekanaje kwamba Isaka, kijana mdogo lakini aliyekuwa na uwezo walau hata kukimbia ili kukwepa kutolewa sadaka, na hasa pale mzee Ibrahimu aliponyosha mkono wake na kutwaa kisu ili amchinje?
Maswali haya na mengineyo yanatupelekea kutambua kwamba kulikuwa na uhusiano wa kipekee kati ya Mungu na Ibrahimu. Uhusiano huu ulijengwa juu ya imani. Mwandishi wa Waraka kwa Waebrania anaonyesha uhusiano huu anapoandika kwamba “Kwa imani Abrahamu alimtoa dhabihu mwanawe Isaka wakati Mungu alipomjaribu. Huyo Abrahamu ndiye aliyekuwa amempokea ahadi ya Mungu, lakini, hata hivyo, alikubali kumtoa dhabihu mwanawe wa pekee, ingawa Mungu alikuwa amemwambia: ‘Wazao wako watatokana na Isaka…'”(Ebr 11:17-19).
Hii ni Kwaresima. Simulizi hili la Ibrahimu linatupatia sisi swali la jinsi tunavyotimiza moja ya masharti ya Kwaresima: Kutoa sadaka. Kutoa sadaka ni mojawapo ya nguzo tatu za Kwaresima. Nyingine ni Sala na Kufunga. Wengi wetu tu wagumu wa kujitoa sadaka na kutoa sadaka kwa sababu tunadhani tu-fukara. Tunasubiri tuwe na vya ziada ili kutoa sadaka. Tunaogopa kufilisika. Ibrahimu ni mfano wetu wa kujitoa na kutoa sadaka hata kwa kidogo tulicho nacho. Tuige pia moyo wa mama mjane maskini ambaye alitoa sadaka ya “Kila kitu alichohitaji kwa kuishi”(Lk 21:1-4). Mungu huwarudishia ukarimu walio wakarimu. Ndivyo inavyotokea katika maisha ya Ibrahimu, kwani Mungu anambariki Ibrahimu kwa kuzidisha uzao wake. Na sababu ni kwamba “Umetii sauti yangu”(Mwa 22:18). Kusikiliza ni kutii.
Katika Injili (Mk 9:2-10) wakati wa tukio la kung’ara sura kwa Yesu Kristo, sauti ya Mungu Baba inasikika ikituambia “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, msikieni yeye”(Mk 2:7). Kuisikia sauti ya Yesu ni kuitii sauti yake. Na kuitii sauti yake ni kufuata masharti yake ya ufuasi. Mojawapo ni “Kujikana, kuchukua msalaba, kumfuata”(Mk 8:34). Ni kujitoa sadaka. Ni sadaka ile ya msalaba. Ni kujikatalia. Na hatuwezi kutimiza hayo bila kwanza kusikiliza na kuutii mwaliko wake.
Hii ni kwaresima. Tunapotafakari juu ya kujitoa kwetu sadaka, hatuna budi nasi kwenda mlimani kama alivyofanya Ibrahimu kule Moria na Yesu kule Tabor. Twende mlimani ili tukakutane na Mungu. Twende mlimani mahali pa sala. Twende mlimani tukamkabidhi Mungu maisha yetu yawe sadaka safi na ya kumpendeza. Twende mlimani tukauone utukufu wa Mungu kama vile Petro, Yakobo na Yohane walivyouona hata wakatamani kubaki pale. Twende mlimani ili tukajifunze sheria za Mungu na kuyasikiliza mafundisho ya manabii. Twende mlimani ili tukamsikilize Kristo na kumpa nafasi ya kutubadilisha maisha na kuyang’arisha kwa utakatifu wake.
 Hii ni Kwaresima. Tunapoanza juma la pili, tuombe neema ya usikivu na utii kwa neno la Mungu ili tuweze kujifunza kujitoa sadaka na kutoa sadaka kwa kidogo tulicho nacho kwani “Yeye (Mungu) ambaye alimtoa Mwanaye kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye?”(Rum 8:32). 

SALA: Ee Bwana utujalie fadhila ya utii ili tuweze kuisikiliza sauti yako. Amina.

Masomo ya Misa Feb 24

Tumsifu Yesu Kristu… Karibu Katika Masomo ya Misa Takatifu 24/02/2024

2024 FEBRUARI 24 JUMAMOSI: JUMA LA 1 LA KWARESIMA
Mt. Flavian 
Kumbukumbu
Urujuani
Zaburi: Juma 1

Somo 1. Kum 26:16-19

Musa aliwaambia watu: Leo hivi akuamuru Bwana, Mungu wako, kuzifanya amri hizi na hukumu; basi uzishike na kuzifanya kwa moyo wako wote na roho yako yote.  Umemwungama Bwana leo, kuwa ndiye Mungu wako, na kuwa yakupasa kutembea katika njia zake, na kushika amri zake na maagizo yake, na hukumu zake, na kusikiza sauti yake; naye Bwana amekuungama hivi leo kuwa taifa iliyotengwa iwe yake yeye, kama alivyokuahidi, na kuwa yakupasa kushika maagizo yake yote; na kuwa atakutukuza juu ya mataifa yote aliyoyafanya kwa sifa, na jina, na heshima, nawe upate kuwa taifa takatifu kwa Bwana, Mungu wako, kama alivyosema.

Wimbo wa Katikati. Zab 119:1-2, 4-5, 7-8

1. Heri walio kamili njia zao,
Waendao katika sheria ya Bwana.
Heri wazitiio shuhuda zake,
Wamtafutao kwa moyo wote. (K)

(K) Heri walio kamili njia zao,
       Waendao katika sheria ya Bwana.
  

2. Wewe umetuamuru mausia yako,
Ili sisi tuyatii sana.
Ningependa njia zangu ziwe thabiti
Nizitii amri zako. (K)

3. Nitakushukuru kwa unyofu wa moyo,
Nikiisha kujifunza hukumu za haki yako.
Nitazitii amri zako,
Usiniache kabisa. (K)

Injili. Mt 5: 43-48

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi; ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki. Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi, mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru; je! nao hawafanyi yayo hayo? Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! nao hawafanyi kama hayo? Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.

TAFAKARI

TUSIBAGUANE KWANI SOTE TU SAWA MBELE ZA MUNGU: Upendo hauna mipaka, haubagui, upendo hauna dini wala kabila mbele ya Mungu. Kama vile Mungu alivyo chanzo na asili ya upendo, naye hatubagui sisi viumbe wake, ndivyo inavyotupasa nasi kutobaguana. Huu ndio wito wa Kristo kwetu. Dhana hii ya kupendana bila ubaguzi inahimizwa na Yesu kwa namna ya pekee katika maelezo aliyowapatia wanafunzi wake. Yesu anawasihi kuwa jambo waliloambiwa ya kuwa wawapende jirani zao na wawachukie adui zao, si sawa. Yesu anaweka upendo kwa wote kwa kuhimiza kuwa wawapende adui zao pia, kwani Mungu aliyetuumba wote, hutoa baraka kwa wote bila ubaguzi. Haya yote ndio tunayoimarishwa na Musa kuwa Bwana Mungu atuamuru kuzishika Amri na hukumu zake. Tumemwungama Bwana kuwa ndiye Mungu na ya kwamba tutafuata maongozi yake. Wapendwa, maisha yetu bila taratibu hayafai na hayaendi, utaratibu tuliopewa na Mungu ni kwamba watu wote tupendane. Katika kupendana tunajaliana, tunamwungama Mungu na tunazishika Amri zake.

SALA: Ee Mwenyezi Mungu, utujalie kuwapenda wote bila ya ubaguzi wowote. Amina.

Masomo ya Misa Feb 23

Tumsifu Yesu Kristu… Karibu Katika Masomo ya Misa 23/02/2023

2024 FEBRUARI 23 IJUMAA: JUMA LA 1 LA KWARESIMA
Mt. Polikarp, Askofu na Shahidi
Urujuani
Zaburi: Juma 1

Somo 1. Eze 18: 21-28

Bwana asema hivi: mtu mbaya akighairi, na kuacha dhambi zake zote alizozitenda, na kuzishika amri zangu zote, na kutenda yaliyo halali na haki, hakika ataishi, hatakufa. Dhambi zake zote alizozitenda hazitakumbukwa juu yake hata moja wapo; katika haki yake aliyoitenda ataishi. Je! Mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu? Asema Bwana Mungu; si afadhali kwamba aghairi, na kuiacha njia yake, akaishi? Bali mwenye haki atakapoghairi, na kuicha haki yake, na kutenda uovu, na kufanya machukizo yote kama yale afanyayo mtu mwovu, je, ataishi? Katika matendo yake yote ya haki aliyoyatenda halitakumbukwa hata mojawapo. Katika kosa lile alilolikosa, na katika dhambi yake aliyoitenda, atakufa. Lakini ninyi mwasema,’ Njia ya Bwana si sawa.’ Sikilizeni sasa, enyi nyumba ya Israeli; je, Njia zangu sizo zilizo sawa? Njia zenu sizo zisizo sawa? Mwenye haki atakapoghairi, na kuiacha haki yake, na kutenda uovu, atakufa katika uovu huo; katika uovu wake alioutenda atakufa. Tena, mtu mwovu atakapoghairi, na kuuacha uovu wake alioutenda, na kutenda yaliyo halali na haki, ataponya roho yake, nayo itakuwa hai. Kwa sababu atafakari, na kughairi, na kuyaacha makosa yake yote aliyoyatenda, hakika ataishi, hatakufa.

Wimbo wa Katikati. Zab 130

1. Ee Bwana, toka vilindini nimekulilia.
Bwana, uisikie sauti yangu.
Masikio yako na yasikilize
Sauti ya dua zangu. (K)

(K) Bwana kama Wewe ungehesabu maovu,
       Ee Bwana, nani angesimama? 
 

2. Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu,
Ee Bwana, nani angesimama?
Lakini kwako kuna msamaha,
Ili Wewe uogopwe. (K)

3. Nimemngoja Bwana, roho yangu imengoja
Na neno lake nimelitumainia.
Nafsi yangu inamngoja Bwana,
Kuliko walinzi waingojavyo asubuhi,
Naam, walinzi waingojavyo asubuhi. (K)

Injili. Mt 5: 20-26

Siku ile Yesu aliwaambia wafuasi wake: Maana nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni. Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiue; na mtu akiua, itampasa hukumu. Bali mimi nawaambieni, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu; na mtu akimfyolea ndugu yake, itampasa baraza; na mtu akimwapiza, itampasa jehanum ya moto. Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako. Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani. Amin, nakuambia: Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho!

TAFAKARI

TUJIPATANISHE NA MUNGU, WAKATI NDIO HUU: Katika ubinadamu wetu, mawazo, maneno na matendo yetu yanaathiriwa na dhambi zetu na inatutenga na Mungu. Kwa njia ya toba tunaghairi dhambi zetu na kumrudia Mungu. Nabii Ezekieli anatueleza juu ya furaha ya Bwana kwa mwovu ambaye ameghairi maovu yake na kumrudia Bwana. Huyu hakika ataishi. Na kwa yule ambaye anaendelea katika uovu wake, ama kwa yule aliyekuwa mtu wa haki na akaacha kutenda mema akatenda maovu atakufa. Huyu ni chukizo kwa Bwana. Yesu anawaonya wafuasi wake ya kwamba haki yao izidi ile ya Waandishi na Mafarisayo ili waupate ufalme wa mbinguni, pia anawaasa juu ya matamanio na makusudio ya kufanya dhambi. Wapendwa, mastahili yetu ya kufika mbinguni yapo ndani ya uwezo na maamuzi yetu ya kufanya mabadiliko. Tunapojikuta wadhambi tujipatanishe na Mungu kwa Sakramenti ya Upatanisho ili tuwe wana wake wapendwa na warithi wa ufalme wa Mungu.

SALA: Ee Mwenyezi Mungu neema ya kuacha njia zetu mbovu na kukurudia Wewe. Amina.

Masomo ya Misa Feb 22

Itukuzwe Damu ya Yesu… Karibu Katika Masomo ya Misa Takatifu 22/02/2024

2024 FEBRUARI 22 ALHAMISI: JUMA LA 1 LA KWARESIMA
UKULU WA PETRO, MTUME
Urujuani
Zaburi: Juma 1

Somo 1. 1 Pet 5:1-4 

Nawasihi wazee walio kwenu, mimi niliye mzee, mwenzi wao, na shahidi wa mateso ya Kristo, na mshirika wa utukufu utakaofunuliwa baadaye; lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiyari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo. Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi. Na Mchungaji mkuu atakapodhihirishwa, mtaipokea taji ya utukufu, ile isiyokauka.

Wimbo wa Katikati. Zab 23

1. Bwana ndiye mchungaji wangu,
Sitapungukiwa na kitu.
Katika malisho ya majani mabichi hunilaza,
Kando ya maji ya utulivu huniongoza. (K)

(K) Bwana ndiye Mchugaji wangu, sitapungukiwa na kitu. 

2. Hunihuisha nafsi yangu, na kuniongoza,
Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake.
Naam nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti,
Sitaogopa mabaya,
Kwa maana wewe upo pamoja nami,
Gongo lako na fimbo yako vyanifariji. (K)

3. Waandaa meza mbele yangu,
Machoni pa watesi wangu.
Umenipaka mafuta kichwani pangu,
Na kikombe changu kinafurika. (K)

4. Hakika wema na fadhili zitanifuata,
Siku zote za maisha yangu,
nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele. (K)

Injili. Mt 16:13-19

Yesu alienda pande za Kaisaria-Filipi, akawauliza wanafunzi wake akasema, Watu hunena Mwana wa adamu kuwa ni nani? Wakasema, Wengine hunena u Yohane Mbatizaji, wengine Eliya, wengine Yeremia au mmojawapo wa manabii. Akawaambia, Nanyi mwaninena mimi kuwa ni nani? Simoni Petro akajibu akasema, Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.  Yesu akajibu, akamwambia, Heri wewe Simoni Bar-yona kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni. Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga Kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda. Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lo lote utakalolifunga duniani, litakuwa limefungwa mbinguni; na lo lote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni.

TAFAKARI

WEWE NDIWE PETRO: Mama Kanisa anatualika kuadhimisha Sikukuu ya Ukulu wa Mt. Petro. Ni Sikukuu inayoadhimisha mamlaka ya Mt. Petro ya kuongoza kondoo wa Bwana Yesu aliokabidhiwa. Ni Sikukuu ya kuadhimisha Kiti-Cathedrali kama alama ya uwezo wa kutawala na kuwaongoza waumini. Ni Sikukuu inayoadhimisha uwajibikaji na utunzaji wa kondoo wa Bwana Yesu aliokabidhiwa Mt. Petro. Ni Sikukuu inayoadhimisha alama ya umoja wa Wakristo inayoonekana kupitia kiti cha Halifa wa Kristo, yaani Mt. Petro. Pia Sikukuu hii hutukumbusha kuwa Mt. Petro na mahalifa wake, yaani Maaskofu wa Kanisa Katoliki, wamewekwa Mawakili wa Yesu hapa duniani. Kazi yao ndio kuyalinda salama na kuyaeneza mafundisho ya Kristo jinsi yeye alivyoliagiza Kanisa lake. Tunapoadhimisha Sikukuu ya Ukulu wa Mt. Petro, tunaalikwa kumwombea Baba Mtakatifu, Halifa wa Mt. Petro ili Mwenyezi Mungu aendelee kumwangazia Roho Mtakatifu aweze kuliongoza Kanisa la Kristo kwa neema na uchaji uliojaa upole, upendo na unyenyekevu. 

SALA: Ee Mungu Mwenyezi umlinde, umkinge na umwongoze Baba Mtakatifu siku zote.

Masomo ya Misa Feb 21

Tumsifu Yesu Kristu. Karibu Katika Masomo ya Misa Takatifu 21/02/2024

2024 FEBRUARI 21 JUMATANO: JUMA LA 1 LA KWARESIMA
Mt. Petro Damiano Askofu na Mwalimu wa Kanisa
Urujuani
Zaburi: Juma 1

Somo 1. Yon 3: 1-10

Neno la Bwana likamjia Yona mara ya pili, kusema, Ondoka uende Ninawi, mji ule mkubwa, ukaihubiri habari nitakayokuamuru. Basi Yona akaondoka, akaenda Ninawi, kama Bwana alivyonena. Basi Ninawi ulikuwa mji mkubwa mno, ukubwa wake mwendo wa siku tatu, Yona akaanza kuuingia mji kwa mwendo wa siku moja, akapaza sauti yake, akasema, Baada ya siku arobaini Ninawi utaangamizwa. Basi watu wa Ninawi wakamsadiki Mungu; wakatangaza kufunga, wakajivika nguo za magunia, tangu yeye aliye mkubwa hata yeye aliye mdogo. Habari ikamfikia mfalme wa Ninawi, naye akaondoka katika kiti chake cha enzi, akavua vazi lake, akajivika nguo za magunia, na kuketi katika majivu. Naye akapiga mbiu, akatangaza habari katika mji wa Ninawi, kwa amri ya mfalme na wakuu wake, kusema. Mwanadamu asionje kitu, wala mnyama wala makundi ya ng’ombe, wala makundi ya kondoo; wasile, wala wasinywe maji; bali na wafunikwe nguo za magunia, mwanadamu na mnyama pia, nao wakamlilie Mungu kwa nguvu, naam, na wageuke, kila mtu akaache njia yake mbaya, na udhalimu ulio mikononi mwake. Ni nani ajuaye kwamba Mungu hatageuka na kughairi, na kuiacha hasira yake kali, ili tusiangamizwe? Mungu akaona matendo yao, ya kuwa wameiacha njia yao mbaya. Basi Mungu akalighairi neno lile baya, ambalo alisema atawatenda; asilitende.

Wimbo wa Katikati. Zab 51:3-4, 12-13, 18-19

1. Ee Mungu, unirehemu,
Sawa na fadhili zako.
Kiasi cha wingi wa rehema zako,
Uyafute makosa yangu. (K)

(K) Moyo uliovunjika na kupondeka,
       Ee Mungu, hutaudharau.


2. Ee Mungu, uniumbie moyo safi,
Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.
Usinitenge na uso wako,
Wala roho yako mtakatifu usiniondolee. (K)

3. Maana hupendezwi na dhabihu, au ningeitoa,
Wewe huridhii sadaka ya kuteketezwa.
Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika,
Moyo uliovunjika na kupondeka. (K)

Injili. Lk 11: 29-32

Makutano walipokuwa wakimkusanyikia, Yesu alianza kusema, Kizazi hiki ni kizazi kibaya; kinatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya Yona. Maana, kama vile Yona alivyokuwa ishara kwa Waninawi, ndivyo atakavyokuwa Mwana wa Adamu kwa kizazi hiki. Malkia wa Kusini ataondoka siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa na hatia; kwa sababu yeye alikuja kutoka nchi za dunia aisikie hekima ya Sulemani; na hapa pana mkubwa kuliko Sulemani. Watu wa Ninawi watasimama siku ya hukumu pamoja na kizazi hiki, nao watakihukumu kuwa na hatia; kwa sababu wao walitubu kwa mahubiri ya Yona, na hapa pana mkubwa kuliko Yona.

TAFAKARI

NI VIZURI KUMSIKILIZA KRISTO KULIKO KUNGOJEA ISHARA: Katika kipindi hiki cha Kwaresma, Mama Kanisa anaendelea kutusihi kufanya mabadiliko. Mama Kanisa anatupa mfano wa watu wa Ninawi ambao kutokana na mahubiri ya Yona wanayabadili maisha yao maovu na wanamgeukia Mungu. Mungu alivyoona matendo yao ya kuwa wamebadilika, alighairi neno lile ya kwamba atawatenda. Kuokoka kwa watu wa Ninawi kunatokana na kubadili mienendo yao. Katika Injili, tunakumbushwa na Yesu kwa mfano wa kizazi kinachotafuta ishara. Yesu anatoa mifano ya Yona aliyekuwa ishara kwa watu wa Ninawi na Malkia wa Kusini ambaye alikuja aisikie hekima ya Sulemani. Yesu anasema kuwa yeye ni mkubwa kuliko Yona na Sulemani. Yeye ndiye mwenye yote katika wote hivyo tumsikilize. Wapendwa Taifa la Mungu, katika ulimwengu tunaoishi tumepata fursa ya kulisikia Neno la Mungu, yatupasa baada ya kulisikiliza, tubadili mienendo yetu tusisubiri mpaka ujio wa pili wa Yesu, tusisubiri mpaka siku ya hukumu. Mabadiliko ni yaanze sasa.

SALA: Ee Bwana, tunakuomba utufanye daima tusiwe watu wa kutafuta ishara, tuwe tayari kubadili mienendo yetu ili tustahilishwe kufika kwako, amina.