Select Page

Masomo ya Misa Machi 15

Tumsifu Yesu Kristu… Karibu Katika Masomo ya Misa 15/03/2024

2024 MACHI 15 IJUMAA: JUMA 4 LA KWARESIMA
Mt. Klementi Hofbauer, Padre
Urujuani
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Hek 2: 1, 12-22

Wasiomsadikia Mungu walisema hivi, huku wakifikiri yasiyo kweli, Zaidi ya hayo na tumwotee mtu wa haki, maana hatuna haja naye, naye yu kinyume cha matendo yetu; atukaripia  ya kama tumeiasi torati, na kutushitaki ya kama tumekosa adabu. Asema ya kwamba anamjua Mungu, na kujiita mtumishi wa Bwana. Ametuwia magombezi ya fikra zetu. Hata kumtazama twaona ni kugumu; maana maisha yake si sawasawa na maisha ya wengine, na mwenendo wake ni wa kigeni. Tunahesabiwa naye kuwa kama madini hafifu; anajitenga na njia zetu kama na uchafu. Wenye haki wasema kuwa mwisho wao ni heri; hujivuna ya kwamba Mungu ndiye baba yake. Haya na tuone kama maneno yake ni kweli; tufanye kujaribu yatakayompata wakati wa mwisho wake; mradi mwenye haki akiwa ni mwana wa Mungu, Yeye atamtegemeza na kumwokoa mikononi mwa adui zake. Na tumhakikishe kwa jeuri na maumivu, ili tujifunze upole wake na kuithibitisha saburi yake akidhulumiwa. Hata tumhukumu auawe mauti ya aibu, maana ataangaliwa sawasawa na maneno yake. Ndivyo walivyosemezana, wakakosea kabisa. Kwa maana uovu wao uliwapofusha; hawakuzijua siri za Mungu; wala hawakuutarajia mshahara wa utakatifu, wala kudhani ya kwamba iko thawabu kwao wenye roho zisizo na hatia.

Wimbo wa Katikati. Zab 34:17-23

1. Uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya,
Aliondoe kumbukumbu lao duniani.
Walilia, naye Bwana akasikia,
Akawaponya na taabu zao zote. (K)

(K) Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo.

2. Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo,
Na waliopondeka roho huwaokoa.
Mateso ya mwenye haki ni mengi,
Lakini Bwana humponya nayo yote. (K)

3. Huihifadhi mifupa yake yote,
Haukuvunjika hata mmoja.
Bwana huzikomboa nafsi za watumishi wake,
Wala hawatahukumiwa wote wamkimbiliao. (K)

Injili. Yn 7: 1-2, 10, 25-30

Wakati ule, Yesu alikuwa akitembea katika Galilaya; maana hakutaka kutembea katika Uyahudi, kwa sababu Wayahudi walikuwa wakitafuta kumwua. Na sikukuu ya Wayahudi, Sikukuu ya vibanda, ilikuwa karibu. Hata ndugu zake walipokwisha kukwea kuiendea sikukuu, ndipo yeye naye alipokwea, si kwa wazi bali kana kwamba kwa siri. Basi baadhi ya watu wa Yerusalemu wakasema, ”Je, Huyu siye wanayemtafuta ili wamwue? Na kumbe! Anena waziwazi, wala hawamwambii neno! Yamkini hao wakuu wanajua hakika ya kuwa huyu ndiye Kristo? Lakini huyu twamjua atokako; bali Kristo atakapokuja hakuna ajuaye atokako.” Basi Yesu akapaza sauti yake hekaluni, akifundisha na kusema, ”Mimi mnanijua, na huko nitokako mnakujua; wala sikuja kwa nafsi yangu; ila yeye aliyenipeleka ni wa kweli, msiyemjua ninyi. Mimi namjua, kwa kuwa nimetoka kwake, naye ndiye aliyenituma.” Basi wakatafuta kumkamata; lakini hakuna mtu aliyeunyosha mkono wake ili kumshika, kwa sababu saa yake ilikuwa haijaja bado.

TAFAKARI

UKWELI UNAUMA: Ni tabia ya wengi kupendelea kusikia/kuambiwa maneno matamu yenye kutusifia na kutuvimbisha vichwa; hatupendi kukaripiwa na kurekebishwa pale tunapofanya sivyo. Katika somo la kwanza tumeona wahusika wanasema “atukaripia ya kama tumeasi torati na kutushitaki ya kama tumekosa adabu.” Katika Injili Wayahudi walikuwa wanamtafuta Yesu ili wamuue. Daima anayesema ukweli na kutetea haki huwa hapendwi na jamii, atachukiwa na hata wakati mwingine atazushiwa jambo la uongo ili tu kumchafulia. Jamii ya leo inapendelea zaidi mambo yanayofuatana na vionjo vyao tu na kuleta furaha ya muda angali roho inaangamia. Mtu yuko radhi adhulumu mali za wengine ili mradi mtaani aonekane ni tajiri, hata kama ni kupoteza uhai wa mtu. Wanasahau kuwa kuna maisha baada ya kifo.  Ndio maana Yesu anasema, ‘yeye aliyempeleka ni wa kweli na ametoka kwake.’ Kila mara Yesu alisimamia ukweli, nasi tunaalikwa tusimamie ukweli hata kama tutachukiwa na wengine.

SALA: Ee Mungu utujalie kusimamia ukweli siku zote.

Masomo ya Misa Machi 14

Tumsifu Yesu Kristu… Karibu Katika Masomo ya Misa 14/03/2024

2024 MACHI 14 ALHAMISI: JUMA 4 LA KWARESIMA
Mt. Matilda wa Ringelheim, Malkia 
Urujuani
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Kut 32:7-14

Bwana akamwambia Musa, Haya! Shuka; kwa maana watu wako uliowatoa katika nchi ya Misri wamejiharibu nafsi zao, wamepotoka upesi kuiacha ile njia niliyowaamuru, wamejifanyizia ndama ya kuyeyusha, wakaiabudu na kuitolea dhabihu, wakasema, Hiyo ndiyo miungu yako, Ee Israeli, iliyokutoa katika nchi ya Misri. Tena Bwana akamwambia Musa, Mimi nimewaona watu hawa, na tazama, ni watu wenye shingo ngumu; basi sasa niache, ili hasira zangu ziwake juu yao, niwaangamize; nami nitakufanya wewe uwe taifa kuu. Musa akamsihi sana Bwana, Mungu wake, na kusema, Bwana, kwa nini hasira zako kuwaka juu ya watu wako uliowaleta kutoka nchi ya Misri kwa uweza mkuu, na kwa mkono wenye nguvu? Kwa nini Wamisri kunena, wakisema, Amewatoa kwa kuwatenda uovu,  ili apate kuwaua milimani, na kuwaondoa watoke juu ya uso wa nchi? Geuka katika hasira yako kali, ughairi uovu huu ulio nao juu ya watu wako. Mkumbuke Ibrahimu, na Isaka na Israeli, watumishi wako, ambao uliwaapia kwa nafsi yako, na kuwaambia, nitazidisha kizazi chenu mfano wa nyota za mbinguni; tena nchi hii yote niliyoinena nitakipa kizazi chenu, nao watairithi milele. Na Bwana akaughairi ule uovu aliosema ya kwamba atawatenda watu wake.

Wimbo wa Katikati. Zab 106:19-23

1. Walifanya ndama huko Horebu,
Wakaisujudia sanamu ya kuyeyusha
Wakaubadili utukufu wao
Kuwa mfano wa ng’ombe mla majani. (K)


 (K)  Ee Bwana unikumbuke mimi,
         Kwa kibali uliyo nayo kwa watu wako. 


2. Matendo ya ajabu katika nchi ya Hamu,
Mambo ya kutisha penye bahari ya Shamu.
Wakamsahau Mungu, mwokozi wao,
Aliyetenda makuu katika Misri. (K)

3. Akasema ya kuwa atawaangamiza,
Kama Musa, mteule wake, asingalisimama,
Mbele zake kama mahali palipobomoka,
Ili aigeuze hasira yake asije akawaharibu. (K)

Injili. Yn 5:31-47

Yesu aliwaambia Wayahudi: Mimi nikijishuhudia mwenyewe, ushuhuda wangu si kweli. Yuko mwingine anayeshuhudia; nami najua ya kuwa ushuhuda wake anaonishuhudia ni kweli. Ninyi mlituma watu kwa Yohane, naye akaishuhudia kweli. Lakini mimi siupokei ushuhuda kwa wanadamu; walakini ninasema haya ili ninyi mpate kuokoka. Yeye alikuwa taa iwakayo na kung’aa, nanyi mlipenda kuishangilia nuru yake kwa muda.
Lakini ushuhuda nilio nao mimi ni mkubwa kuliko ule wa Yohane; kwa kuwa zile kazi alizonipa Baba ili nizimalize, kazi hizo zenyewe ninazozitenda, zanishuhudia ya kwamba Baba amenituma. Naye Baba aliyenipeleka amenishuhudia. Sauti yake hamkuisikia wakati wo wote, wala sura yake hamkuiona. Wala neno lake hamnalo likikaa ndani yenu, kwa kuwa ninyi hammwamini yule aliyetumwa na yeye.
Mwayachunguza maandiko, kwa sababu mnadhani kwamba ninyi mna uzima wa milele ndani yake; na hayo ndiyo yanayonishuhudia. Wala hamtaki kuja kwangu mpate kuwa na uzima. Mimi siupokei utukufu kwa wanadamu. Walakini nimewajua ninyi ya kuwa hamna upendo wa Mungu ndani yenu. Mimi nimekuja kwa jina la Baba yangu, wala ninyi hamnipokei; mwingine akija kwa jina lake mwenyewe, mtampokea huyo.
Mwawezaje kuamini ninyi mnaopokeana utukufu ninyi kwa ninyi, na utukufu ule utokao kwa Mungu aliye wa pekee hamwutafuti? Msidhani kwamba mimi nitawashitaki kwa Baba; yuko anayewashitaki, ndiye Musa, mnayemtumaini ninyi. Kwa maana kama mngalimwamini Musa, mngeniamini mimi; kwa sababu yeye aliandika habari zangu. Lakini msipoyaamini maandiko yake, mtayaamini wapi maneno yangu?

TAFAKARI

MAFANIKIO DAIMA YANAHITAJI MSIMAMO: Mwanadamu mara nyingi hupenda kujaribu na kubahatisha mambo na hii wakati mwingine hupelekea yeye kujikuta amepoteza vyote. Somo la kwanza tumeona Waisrael wanapotoka na kumwacha Mungu na kugeukia miungu mingine. Katika Injili Yesu anaweka bayana na kusema, “mimi nimekuja kwa jina la Baba yangu wala hamnipokei, mwingine akija kwa jina lake mwenyewe mtampokea.” Wahenga wanasema, “miluzi mingi humpotezea mbwa mwelekeo” au “mshika mawili kwa pupa yote humponyoka.” Tunashuhudia siku hizi kila uchwao makanisa yanaibuka kila kona na kila mmoja anatumia Biblia lakini katika uhalisia ni miradi kwa manufaa binafsi ya kujitafutia hela. Mwanadamu amekosa mwelekeo na hata mafanikio ya kubaki imara kwa imani kwa Mungu hamna, amekosa msimamo, leo yupo Katoliki, kesho yuko kwingineko. Kutangatanga kumekuwa kwingi.

SALA: Yesu Mwema, utuwezeshe tudumu imara kwa imani Katoliki.

Masomo ya Misa Machi 13

Tumsifu Yesu Kristu… Karibu Katika Masomo ya Misa 13/03/2024

2024 MACHI 13 JUMANNE: JUMA 4 LA KWARESIMA
Mt. Eufrasia
Urujuani
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Isa 49: 8-15

Bwana asema hivi, Wakati uliokubalika nimekujibu, na siku ya wokovu nimekusaidia; nami nitakuhifadhi, nitakutoa uwe agano la watu hawa, ili kuiinua nchi hii, na kuwaridhisha urithi uliokuwa ukiwa; kuwaambia waliofungwa, Haya, tokeni; na hao walio katika giza, Jionyesheni. Watajilisha katika njia, na juu ya majabali watapata malisho. Hawataona njaa, wala hawataona kiu; hari haitawapiga, wala jua; kwa maana yeye aliyewarehemu atawatangulia, naam, karibu na chemchemi za maji atawaongoza. Nami nitafanya milima yangu yote kuwa njia, na njia kuu zangu zitatukuzwa zote. Tazama, hawa watakuja kutoka mbali; na tazama, hawa kutoka kaskazini, na kutoka magharibi, na hawa kutoka nchi ya Sinimu. Imbeni, enyi mbingu; ufurahi, Ee nchi; pazeni sauti ya kuimba, enyi milima; kwa kuwa Bwana amewafariji watu wake, naye atawahurumia watu wake walioteswa. Bali Sayuni alisema, Yehova ameniacha, Bwana amenisahau. Je! Mwanamke aweza kumsahau mtoto wake amnyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe.

Wimbo wa Katikati. Zab 145:8-9, 13-14, 17-18

1. Msifu Bwana, Ee Yerusalemu;
Msifu Mungu wako, Ee Sayuni.
Maana ameyakaza mapingo ya malango yako,
Amewabariki wanao ndani yako. (K)

(K) Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma.

2. Huipeleka amri yake juu ya nchi,
Neno lake lapiga mbio sana.
Ndiye atoaye theluji kama sufu,
Huimwaga barafu yake kama majivu. (K)

3. Humhubiri Yakobo neno lake,
Na Israeli amri zake na hukumu zake.
Hakulitendea taifa lo lote mambo kama hayo,
Wala hukumu zake hawakuzijua. (K)     

Injili. Yn 5: 17-30

Yesu aliwajibu Wayahudi: Baba yangu anatenda kazi hata sasa, nami ninatenda kazi. Basi kwa sababu hiyo Wayahudi walizidi kutaka kumwua, kwa kuwa hakuivunja sabato tu, bali pamoja na hayo alimwita Mungu Baba yake, akijifanya sawa na Mungu. Basi Yesu akajibu, akawaambia, Amin, amin, nawaambia, mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda; kwa maana yote ayatendayo yeye, ndiyo ayatendayo Mwana vilevile. Kwa kuwa Baba ampenda Mwana, naye humwonyesha yote ayatendayo mwenyewe; hata na kazi kubwa zaidi kuliko hizi atamwonyesha, ili ninyi mpate kustajaabu. Maana kama Baba awafufuavyo wafu na kuwahuisha, vivyo hivyo na Mwana awahuisha wale awatakao. Tena Baba hamhukumu mtu ye yote, bali amempa Mwana hukumu yote, ili watu wote wamheshimu Mwana kama vile wanavyomheshimu Baba. Asiyemheshimu Mwana hamheshimu Baba aliyempeleka. Amin, amin, nawaambia, Yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani. Amin, amin, nawaambia, Saa inakuja, na sasa ipo, wafu watakapoisikia sauti ya Mwana wa Mungu, na wale waisikiao watakuwa hai.
Maana kama vile Baba alivyo na uzima nafsini mwake, vivyo hivyo alimpa na Mwana kuwa na uzima nafsini mwake. Naye akampa amri ya kufanya hukumu kwa sababu ni Mwana wa Adamu. Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu. Mimi siwezi kufanya neno mwenyewe; kama nisikiavyo ndivyo nihukumuvyo; na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka.

TAFAKARI

TUSIFANYE MAAMUZI KWA HARAKA: Kuna watu wakisikia jambo hupenda kuchukua maamuzi ya haraka bila hata kufanya uchunguzi wa kutosha. Wayahudi walipanga kumuua Yesu japo alikuwa amefanya mambo machache tu pale kwao. Hapa ni kuchukua maamuzi ya haraka. Katika matukio mengine, wapo waliochomwa moto kwa tuhuma za wizi tena wa vitu vidogo tu-simu/kuku, huku ni kujichukulia sheria mkononi na kuchukua maamuzi ya haraka yasiyo na busara, hata kama mtu katenda kosa, kuna sheria na taratibu za kumwajibisha/kumwadhibu na sio kuua. Kuna usemi wa Wahenga usemao “jambo usilolijua ni kama usiku wa kiza.” Hapa tujifunze kutopenda kuchukua maamuzi ya haraka na hasa yale yahusuyo kuondoa uhai, yapo yanayotakiwa kutatuliwa kwa haraka japo busara lazima iwepo, mfano katika janga la moto ili kuokoa uhai na vitu, lazima uharaka uwepo. Je, mara ngapi tumejikuta hata tunawakwamisha wenzetu kiimani kutokana na uharaka tunaokuwa nao hata katika kutatua changamoto za kiimani.

SALA: Yesu Mwema, tuwezeshe kuwa na busara katika maamuzi yetu.

Masomo ya Misa Machi 12

Tumsifu Yesu Kristu. Karibu Katika Masomo ya Misa 12/03/2024

2024 MACHI 11 JUMANNE: JUMA 4 LA KWARESIMA
Mt. Bernad wa Karinola 
Urujuani
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Eze 47: 1– 9, 12

Malaika alinileta mpaka lango la nyumba; na tazama, maji yalitoka chini ya kizingiti cha nyumba, kwa njia ya mashariki, maana upande wa mbele wa nyumba ulielekea upande wa mashariki; nayo maji yakashuka toka chini ya upande wa kuume wa nyumba, upande wa kusini wa madhabahu. Ndipo akanileta nje kwa njia ya lango upande wa kaskazini, akanizungusha kwa njia ya nje mpaka lango la nje, kwa njia yake iliyoelekea mashariki; na tazama, maji yalitoka upande wa kuume. Na alipotoka mtu yule, mwenye uzi wa kupimia mkononi mwake, kwenda masharikini, akapima dhiraha elfu, akanivusha maji yale; maji yakafika mpaka viweko vya miguu. Kisha akapima dhiraha elfu, akanivusha maji yale, maji yakafika mpaka magoti. Kisha akapima dhiraha elfu, akanivusha, maji yakafika mpaka viuno. Kisha akapima dhiraha elfu, yakawa mto nisioweza kuuvuka; maana maji yamezidi, maji ya kuogelea, mto usiovukika. Akaniambia, ”Mwanadamu, je, Umeona haya?” Kisha akanichukua, akanirudisha mpaka ukingo wa mto. Basi nikiisha kurudi, tazama, kando ya ukingo wa mto ilikuwapo miti mingi sana, upande huu na upande huu. Ndipo akaniambia, ”Maji haya yanatoka kwenda pande za nchi ya mashariki, nayo yanashuka mpaka Araba, na kuingia katika bahari; maji yatokezwayo yataingia baharini, na maji yake yataponyeka. Tena itakuwa, kila kiumbe hai kisongamanacho, kila mahali itakapofika mito hiyo, kitaishi; kutakuwapo wingi mkubwa wa samaki, kwa sababu maji haya yamefika huko; maana maji yale yataponyeka, na kila kitu kitaishi po pote utakapofikilia mto huo. Na karibu na mto, juu ya ukingo wake, upande huu na upande huu, utamea kila mti wa chakula, ambao majani yake hayatanyauka, wala matunda yake hayatatindika kamwe; utatoa matunda mapya kila mwezi, kwa sababu maji yake yanatoka mahali patakatifu; na matunda yake yatakuwa ni chakula; na majani yake yatakuwa ni dawa.

Wimbo wa Katikati. Zab 46:2-6, 8-9

1. Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu,
Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.
Kwa hiyo hayutaogopa ijapobadilika nchi,
Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. (K)

(K) Bwana wa majeshi yu pamoja nasi,
       Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.


2. Kuna mto, vijito vyake vyaufurahisha mji wa Mungu,
Patakatifu pa maskani zake Aliye juu.
Mungu yu katikati yake hautatetemeshwa;
Mungu atausaidia asubuhi na mapema. (K)

3. Bwana wa majeshi yu pamoja nasi,
Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.
Njoni myatazame matendo ya Bwana,
Jinsi alivyofanya ukiwa katika mchi. (K)

Injili. Yn 5: 1-16

Baada ya hayo palikuwa na sikukuu ya Wayahudi; naye Yesu akakwea kwenda Yerusalemu. Na huko Yerusalemu penye mlango wa kondoo pana birika, iitwayo kwa Kiebrania Bethzatha, nayo ina matao matano. Ndani ya hayo jamii kubwa ya wagonjwa walikuwa wamelala, vipofu, viwete, nao waliopooza. Na hapa palikuwa na mtu, ambaye amekuwa hawezi muda wa miaka thelathini na minane. Yesu alipomwona huyu amelala, naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, ”Wataka kuwa mzima?” Yule mgonjwa akamjibu, ”Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu.” Yesu akamwambia, ”Simama, jitwike godoro lako, uende.” Mara yule mtu akawa mzima, akajitwika godoro lake, akaenda. Nayo ilikuwa ni Sabato siku hiyo. Kwa sababu hiyo Wayahudi wakamwambia yule aliyeponywa, ”Leo ni sabato, wala si halali kwako kujitwika godoro.” Akawajibu, ”Yeye aliyenifanya kuwa mzima ndiye aliyeniambia, ‘Jitwike godoro lako, uende.”’ Basi wakamwuliza, ‘Yule aliyekuambia, ‘Jitwike, uende, ni nani? ”’Lakini yule mtu aliyeponywa hakumjua ni nani; maana Yesu alikuwa amejitenga, kwa sababu palikuwa na watu wengi mahali pale. Baada ya hayo Yesu akamkuta ndani ya hekalu, akamwambia, ”Angalia, umekuwa mzima; usitende dhambi tena, lisije likakupata jambo lililo baya zaidi.” Yule mtu akaenda zake, akawapasha habari Wayahudi ya kwamba ni Yesu aliyemfanya kuwa mzima. Kwa sababu hiyo Wayahudi wakamwudhi Yesu, kwa kuwa alitenda hayo siku ya Sabato.

TAFAKARI

TUFURAHIE BARAKA NA MAFANIKIO YA WENGINE: Mungu hujifunua kwetu hatua kwa hatua, wakati mwingine hutumia njia ngumu kufanya hivyo na twaweza tusitambue, tunachoalikwa kufanya ni sisi kutoa ushiriki wetu kama Mt. Augustino alivyosema, “Yeye aliyekuumba wewe, bila ya wewe, hatakukomboa wewe bila ya wewe.” Huyu mgonjwa aliyeponywa alitoa ushiriki wake, Yesu alipomuuliza alijibu “sina mtu wa kunitia birikani” na alipoambiwa “simama jitwike godoro lako uende” hakubisha, alitekeleza mara moja na kizuri kingine alichofanya baada ya kupona, alirudi hekaluni kushukuru na hii ilimfanya akakamilisha uponyaji wake. Wayahudi hawakufurahishwa na kuponywa kwake, ndio maana wanamhoji juu ya kubeba godoro siku iliyokatazwa. Tupo ambao hata tukitendewa wema haturudi kushukuru, ndo imetoka hivyo. Kwenye maparokia mengi, watoto wakishapata Kipaimara, Kanisani hawakanyagi tena, labda utamuona siku ya kufunga ndoa. Tujifunze kuwa na maisha endelevu ya kiroho, tujue hamna likizo, mwisho wa hatua moja ni mwanzo wa hatua nyingine.

SALA: Ee Mungu utujkalie neema ya kufurahia mafanikio ya wengine.

Masomo ya Misa Machi 11

Tumsifu Yesu Kristu… Karibu Katika Masomo ya Misa 11/03/2024

2024 MACHI 11 JUMATATU: JUMA 4 LA KWARESIMA
Mt. Teresa Margaret Redi 
Urujuani
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Isa 65:17-21

Bwana asema: ”Tazama, mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo; maana, tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha. Nami nitaufurahia Yerusalemu, nitawaonea shangwe watu wangu; sauti ya kulia haitasikiwa ndani yake tena, wala sauti ya kuomboleza. Hatakuwapo tena mtoto wa siku chache, wala mzee asiyetimia siku zake; kwa maana mtoto atakufa mwenye umri wa miaka mia; bali mtenda dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa. Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. 

Wimbo wa Katikati. Zab 30:2, 3-5, 11-13

1. Ee Bwana, nitakutukuza kwa maana umeniinua,
Wala hukuwafurahisha adui zangu juu yangu.
Umeniinua nafsi yangu,
Ee Bwana, kutoka kuzimu.
Umenihuisha na kunitoa
Miongoni mwao washukao shimoni. (K)

(K) Nitakutukuza, ee Bwana, kwa maana umeniinua.

2. Mwimbieni Bwana zaburi,
Enyi watauwa wake.
Na kufanya shukrani.
Na kumbukumbu la utakatifu wake.
Maana ghadhabu zake ni za kitambo kidogo,
Katika radhi yake mna uhai.
Huenda kilio huja kukaa usiku,
Lakini asubuhi huwa furaha. (K)

3. Ee Bwana, usikie, unirehemu,
Bwana, uwe msaidizi wangu.
Uligeuza matanga yangu kuwa machezo;
Ulinivua gunia, ukanivika furaha.
Ee Bwana, Mungu wangu,
Nitakushukuru milele. (K)

Injili. Yn 4:43-54

Wakati ule, Yesu aliondoka Samaria, akaenda Galilaya. Kwa maana Yesu mwenyewe alishuhudia ya kwamba nabii hapati heshima katika nchi yake mwenyewe. Basi alipofika Galilaya, Wagalilaya walimpokea; kwa kuwa wameyaona mambo yote aliyoyatenda huko Yerusalemu wakati wa sikukuu; maana hao nao waliiendea sikukuu. Basi alifika tena Kana ya Galilaya, hapo alipoyafanya yale maji kuwa divai. Na palikuwa na diwani mmoja ambaye mwanawe hawezi huko Kapernaumu. Huyo aliposikia ya kwamba Yesu amekuja kutoka Uyahudi mpaka Galilaya, alimwendea, akamsihi ashuke na  kumponya mwanawe; Kwa maana alikuwa kufani. Basi Yesu akamwambia, ”Msipoona ishara na maajabu hamtaamini kabisa?” Yule diwani akamwambia, ”Bwana, ushuke asijakufa mtoto wangu.” Yesu akamwambia, ”Enenda; mwanao yu hai.” Mtu yule akalisadiki lile neno aliloambiwa na Yesu, naye akashika njia. Hata alipokuwa akishuka, watumwa wake walimlaki, wakisema ya kwamba mtoto wake yu hai. Basi akawauliza habari ya saa alipoanza kuwa hajambo; nao wakamwambia, jana, saa saba, homa ilimwacha. Basi babaye akafahamu ya kuwa ni saa ile ile alipoambiwa na Yesu, ”Mwanao yu hai.” Akaamini yeye na wote wa nyumbani mwake. Hiyo ni ishara ya pili aliyoifanya Yesu, alipokuwa ametoka Uyahudi kufika Galilaya.

TAFAKARI

MAZOEA HUJENGA KILEMA: Ukichunguza maisha ya viumbe kama Punda, Nyumbu, Panya n.k wanavyopita eneo moja mara nyingi hujenga mazoea na hata wanapokuwa wanapita huweza hata kupinda kona bila kuangalia kwa jinsi walivyozoea. Hii ni kutokana na mazoea ya muda mrefu. Hata mwanadamu ana hulka ya namna hii, anapokuwa mara kwa mara anafanya jambo, hujenga mazoea na wakati mwingine huishia katika dharau, kutotoa heshima stahiki na kujisemea, ‘oh huyu si nilikuwa nae jana! huyu si nilisoma nae! huyu si mtoto wa fulani! Hii inachangiwa na watu kumjua mhusika kwa undani hivyo kwamba wanavyojenga dharau hata akisema jambo zuri linapuuzwa. Mfano; Padre anaweza akaanza kuhamasisha waamini ili wajenge kanisa zuri lakini usishangae wakaanza kumbeza kwa kusema, ‘mbona kwao tunakufahamu, hamna hata nyumba nzuri!’ wazo lake litapuuzwa wala halitatiliwa maanani. Yesu akasema “Nabii hapokelewi kwao” Je mara ngapi tumekwamisha maendeleo ya Kanisa kwa kubeza wahusika kisa tunawafahamu?

SALA: Bwana tunakuomba utujalie neema ya kupokeana katika maisha yetu na kukubali mawazo ya wengine.

Masomo ya Misa Machi 10

Tumsifu Yesu Kristu… Karibu Katika Masomo ya Misa 10/03/2024

2024 MACHI 10 JUMAPILI: DOMINIKA 4 YA KWARESIMA
Urujuani
Zaburi: Juma 4

Somo 1. 2Nya 36 :14-16, 19-23

Wakuu wote wa makuhani, na watu, wakakosa mno sawasawa na machukizo yote ya mataifa; wakainajisi nyumba ya Bwana aliyoitakasa katika Yerusalemu. Naye Bwana, Mungu wa baba zao, akatuma kwao kwa mikono ya wajumbe wake, akiondoka mapema, na kutuma; kwa sababu aliwahurumia watu wake, na makao yake; lakini waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake; na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya Bwana juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya.
Wakaiteketeza nyumba ya Mungu, wakaubomoa ukuta wa Yerusalemu, wakayateketeza kwa moto majumba yake yote, wakaviharibu vyombo vyake vyote vya thamani. Na wale waliookoka na upanga akawachukua mpaka Babeli; wakamtumikia yeye na wanawe hata kulipoingia milki ya Uajemi; ili kulitimiza neno la Bwana kwa kinywa cha Yeremia, hata nchi itakapofurahia sabato zake; kwa maana siku zote ilipokaa ukiwa ilishika sabato, kutimiza miaka sabini.
Ikawa katika mwaka wa kwanza wa Koreshi, mfalme wa Uajemi, ili kwamba neno la Bwana alilolisema kwa kinywa cha Yeremia lipate kutimizwa, Bwana akamwamsha roho yake Koreshi, mfalme wa Uajemi, hata akapiga mbiu katika ufalme wake wote, akaiandika pia, akisema, Koreshi, mfalme wa Uajemi asema  hivi; Bwana, Mungu wa Mbinguni, amenipa  falme  zote za dunia; naye ameniagiza nimjengee nyumba katika Yerusalemu, ulioko Yuda. Basi kila mtu katika ninyi nyote mlio watu wake, Bwana, Mungu wake, na awe pamoja naye, na akwee.

Wimbo wa Katikati. Zab 137:1-6

1. Kando ya mito ya Babeli ndiko tulikoketi,
Tukalia tulipoikumbuka Sayuni.
Katika miti iliyo katikati yake
Tulivitundika vinubi vyetu. (K)

(K) Ulimi wangu na ugandamane
       Na kaakaa la kinywa changu, nisipokumbuka.


2. Maana huko waliotuchukua mateka
Walitaka tuwaimbie;
Na waliotuonea walitaka furaha;
Tuimbieni baadhi ya nyimbo za Sayuni.(K)

3. Tuuimbeje wimbo wa Bwana
Katika nchi ya ugeni?
Ee Yerusalemu, nikikusahau wewe,
Mkono wangu wa kuume na usahau. (K)

4. Ulimi wangu na ugandamane
Na kaakaa la kinywa changu, nisipokukumbuka.
Nisipoikuza Yerusalemu
Zaidi ya furaha yangu iliyo kuu. (K)

Somo 2. Efe 2 :4-10

 Mungu, kwa kuwa ni mwingi wa rehema, kwa mapenzi yake makuu aliyotupenda: hata wakati ule tulipokuwa wafu kwa sababu ya makosa yetu; alituhuisha pamoja na Kristo; yaani, mmeokolewa kwa neema. Akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu;  ili katika zamani zinazokuja audhihirishe wingi wa neema yake upitao kiasi kwa wema wake kwetu sisi katika Kristo Yesu. Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu. Maana tu kazi yake, tuliumbwa katika Kristo Yesu, tutende matendo mema, ambayo tokea awali Mungu aliyatengeneza ili tuenende nayo.

Injili.Yn 3 :14-21

Yesu alimwambia Nikodemo: Kama vile Musa alivyomwinua yule nyoka jangwani, vivyo hivyo Mwana wa Adamu hana budi kuinuliwa; ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele katika yeye.
Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe wa pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.
Na hili ndiyo hukumu; ya kuwa nuru imekuja ulimwenguni, na watu wakapenda giza kuliko nuru; kwa maana matendo yao yalikuwa maovu. Maana kila mtu atendaye mabaya huichukia nuru, wala haji kwenye nuru, matendo yake yasije yakakemewa. Bali yeye aitendaye kweli huja kwenye nuru, ili matendo yake yaonekane wazi ya kuwa yametendwa katika Mungu.

TAFAKARI

WEMA WA MUNGU HAUSHINDWI NA UOVU WA MWANADAMU: Mungu amemuumba mwanadamu kusudi aunganike naye milele. Hii ni kwa sababu ya upendo wake mkubwa usio na mwisho. Mwanadamu anapoingia katika hali ya uasi Mungu anaendelea kumfikiria na kumtafuta. Pamoja na kwamba wakati mwingine Mungu humwadhibu mwanadamu kwa sababu ya uovu wake, hukumu yake haiushindi upendo wake. Ndiyo maana Mama Kanisa anatupatia fursa kila mwaka ya kupita katika kipindi cha toba kusudi kustahilishwa kushirikishwa furaha ya upendo wake. Antifona ya Mwanzo ya Dominika hii inayoitwa Dominika ya Furaha inatualika katika furaha hiyo ikisema: “Furahi Jerusalemu: mshangilieni ninyi nyote mmpendao: furahini, ninyi nyote mliao kwa ajili yake, mpate kunyonya, na kushibishwa kwa maziwa ya faraja zake”. Tunaalikwa kufurahi sababu katika Yeye tutafarijiwa, tutanyonya maziwa na kushibishwa, ishara ya kuwa hai tena.
Somo la kwanza linatuonesha kuwa hukumu ya Mungu ni ya haki sababu ya uovu wetu; haki ya hukumu yake inaambatana na huruma yake, ufunuo wa upendo wake usio na kikomo kwani wema wake haushindwi na uovu wa mwanadamu. Dhambi zetu haziufifishi wema wake wala kumfanya Yeye kukata tamaa. Hii ni kwa sababu upendo wake mkuu wadumu milele. Mwenyezi Mungu aliwatumia wakuu wa wote na makuhani wa taifa ya Israeli wajumbe ili kugeuza mienendo yao “kwa sababu aliwahurumia watu wake, na makao yake; lakini waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake; na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya Bwana juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponywa”.
Mwanadamu katika hali ya uhasi mkuu hivi anatangaziwa wokovu wa Mungu kupitia Koreshi mfalme wa Uajemi. Hapa ndipo urefu na upana wa upendo wa Mungu unapojidhihirisha. Maneno yake kupitia kinywa cha Nabii anasema: “Je! Mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu? … si afadhali kwamba aghairi, na kuiacha njia yake akaishi?” (Eze 18:23). Mungu hafurahii hali yetu ya uovu. Hii ni kwa sababu sisi tulio matunda ya kazi yake njema ya uumbaji ametuumba tukiwa wakamilifu na wenye sura na mfano wake. Hali ya dhambi inatuziba na kushindwa kuionesha haiba hii; inaturubuni tuache kuutangaza ukuu wa Mungu unaofichika ndani mwetu.
Kilele cha upendo wake huu mkuu ni katika nafsi ya Kristo, mwanaye mpendwa, Nafsi ya pili ya Utatu Mtakatifu sana. Yeye analetwa kwetu kama njia ya wokovu ambayo kwayo wote watakaomwamini wataokolewa. Kristo anaonesha namna ya kuujongea wokovu huo. Anamwambia Nikodemo katika somo la Injili: “Kama vile Musa alivyomwinua yule nyoka jangwani, vivyo hivyo Mwana wa Adamu hana budi kuinuliwa; ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele katika yeye.” Mwana wa Adamu atainuliwa juu msalabani ishara ya wokovu wetu. Tendo hili la kuinuliwa kutoka katika ardhi ni ishara ya kuinua macho ya mioyo yetu kutoka maisha ya kawaida ya dunia hii na kwenda juu.
Kuwa juu ni ishara ya kuungana na Mungu na kuyatazama malimwengu katika jicho la kimungu. Hiyo ndiyo imani ambayo Kristo anatualika tuwe nayo katika Yeye. Maisha yake ya hadharani hapa duniani yametufunulia namna mbalimbali za kuyakabili maisha katika jicho la Mungu. Ni wazi kwamba namna hiyo kwa walioangalia katika jicho la kidunia waliona ni chukizo kiasi cha kumwadhibu kwa namna hiyo ya kikatili. Lakini namna yao ya kumwadhibu kwa kumwinua juu ya msalaba ni sababu ya wokovu wetu na ufunuo wa upendo wa Mungu kwetu. Tunapoelekeza macho yetu katika msalalaba na kuungana naye huku tukiyaangalia malimwengu kutoka juu tutapata nguvu ya kupita katika ulimwengu kinzani huku tukielekea kwa Mungu.
Injili Takatifu inataadharisha pia juu ya upande wa pili, yaani kwa wale wasioamini. Neno la Mungu linasema: “asiyeamini amekwisha hukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.” Asiyeamini ni yeye ambaye hapandi pamoja na Mwana pekee wa Mungu juu msalabani na kuyaangalia mambo katika namna ya Mungu. Huyu ni yule ambaye anatawaliwa na mienendo ya ulimwengu mamboleo ambao unaendelea kumpatia mwanadamu mwenye ukomo wa uelewa matumaini bandia juu ya ujuzi wake. Hukumu inamjia kwa sababu “nuru imekuja ulimenguni, na watu wakapenda giza kuliko nuru; kwa maana matendo yao yalikuwa maovu.” Mwanadamu anayeacha kumtazama Yeye aliyeinuliwa juu msalabani anaishia katika giza kwa sababu anabaki katika ukomo wa kuona ukweli wote.
Mwanadamu ana ukomo katika uelewa wake. Hivyo ni pale tu mwanadamu anapounganika na Mungu mwenye uwezo wa kujua na kuona yote ataweza kufanikiwa. Leo hii tunashuhudia jamii ambayo haitaki kuinua macho juu na kuyaelewa yote katika muono wa kimungu. Matokeo yake tunakuwa ni kizazi chenye uelewa nusunusu wa mambo mbalimbali yamhusuyo mwanadamu. Masuluhisho mengi hufanyika nusunusu na wakati mwingine kutawaliwa na ubinafsi au kutafuta maslahi ya mtu mmoja mmoja. Kila mmoja anakuwa ni mjuaji na matokeo yake ni mafarakano na kutoelewana kati yetu. Hatuwezi kamwe kutoka katika hali hii kama tusipoitazama hii nuru inayotuzukia katika Yeye aliyeinuliwa juu msalabani.
Mtume Paulo anatukumbusha haiba yetu kwamba “tumeokolewa kwa neema.” Hali hii ya neema inatutenga na ulimwengu na kutuunganisha na Kristo aliyeinuliwa msalabani. Ni zawadi ya Mungu kwetu anayotupatia bila hata kustahili. Hii ni kwa sababu hata tulipokuwa katika hali ya dhambi kwa mastahili yetu “alituhuisha pamoja na Kristo.” Sakramenti ya ubatizo inatupatia uzima mpya. Tunazaliwa mara ya pili na kujazwa neema ya Mungu ndani mwetu, neema ambayo inatufanya kuwa wana warithi wa Mungu. Mwitikio wetu unapaswa kuwa ni shukrani kwa Mungu. Mzaburi anatuonesha namna njema ya kushukuru kwa njia ya kuyakumbuka matendo ya Mungu. Israeli alipokumbuka hali yake akiwa utumwani Babeli na hali yake ya sasa katika uhuru anaimba kwa shukrani akisema: “Ulimi wangu na ugandamane na kaakaa la kinywa  changu, nisipokukumbuka”
Kipindi cha Kwaresima ni fursa nyingine kwetu ya kubadili mwelekeo wa maisha kwa ajili ya wokovu wetu sote. Tuikumbuke aiba yetu kwamba tumeinuliwa juu kutoka katika ulimwengu huu. Ni kipindi ambacho tunaalikwa kuyainua macho yetu juu na kuelekeza kwa Mungu kwa kumtazama Yeye waliyemchoma. Kwake tunaweza kumwona Mungu ambaye amejinyenyekesha katika namna ya ajabu kwa ajili ya wokovu wangu mimi na wewe. Msalabani anatufundisha unyenyekevu, msamaha, utii, uvumilivu na zaidi ya yote upendo fadhila ambazo kwazo zinaimarisha mahusiano yetu na Mungu na pia mahusiano yetu sisi kwa sisi. Tendo letu la kumtazama Kristo msalabani litaufunua upendo wa Mungu na hivyo tunafanywa kuwa sababu ya wokovu kwa ulimwengu wote. Upendo wa Mungu kwetu ni mkubwa mno na kamwe haushindwi wala kufifishwa na uovu wa mwanadamu.

SALA: Ee Bwana utujalie neema ili macho yetu yaelekee zaidi upendo wako.