Mt. Didas wa Sevila, Mtawa
Kijani
Zaburi: Juma 1
SOMO I: Ufu. 1:1-4; 2:1-5
Ufunuo wa Yesu Kristo, aliopewa na Mungu awaonyeshe watumwa wake mambo ambayo kwamba hayana budi kuwako upesi; naye akatuma kwa mkono wa malaika akamwonyesha mtumwa wake Yohane; aliyelishuhudia neno la Mungu, na ushuhuda wa Yesu Kristo, yaani, mambo yote aliyoyaona. Heri asomaye na wao wayasikiao maneno ya unabii huu, na kuyashika yaliyoandikwa humo; kwa maana wakati u karibu. Yohane, kwa yale makanisa saba yaliyoko Asia: neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwake yeye aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja; na zitokazo kwa roho saba walioko mbele ya kiti chake cha enzi. Nilisikia Bwana ananiambia: “Kwa malaika wa kanisa lililoko Efeso andika; ‘haya ndiyo anenayo yeye azishikaye hizo nyota saba katika mkono wake wa kuume, yeye aendaye katikati ya vile vinara saba vya dhahabu. Nayajua matendo yako, na taabu yako, na subira yako, na ya kuwa huwezi kuchukuliana na watu wabaya, tena umewajaribu wale wajiitao mitume, nao sio, ukawaona kuwa waongo; tena ulikuwa na subira na kuvumilia kwa ajili ya jina langu, wala hukuchoka. Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza. Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza.’”
Wimbo Wa Katikati: Zab. 1:1-4, 6
- Heri mtu yule asiyekwenda
Katika shauri la wasio haki;
Wala hakusimama katika njia ya wakosaji;
Wala hakuketi barazani pa wenye mizaha.
Bali sheria ya Bwana ndiyo impendezayo,
Na sheria yake huitafakari mchana na usiku.
(K) Yeye ashindaye, nitampa matunda ya mti wa uzima.
- Naye atakuwa kama mti uliopandwa
Kandokando ya vijito vya maji,
Uzaao matunda yake kwa majira yake,
Wala jani lake halinyauki;
Na kila alitendalo litafanikiwa. (K) - Sivyo walivyo wasio haki;
Nao ni kama makapi yapeperushwayo na upepo.
Kwa hiyo wasio haki hawatasimama hukumini,
Wala wakosaji katika kusanyiko la wenye haki. (K)
INJILI: Lk. 18:35-43
Yesu alipokaribia Yeriko, mtu mmoja kipofu alikuwa ameketi kando ya njia, akiomba sadaka; na alipowasikia makutano wakipita, aliuliza, “Kuna nini?” Wakamwambia, “Yesu wa Nazareti anapita.” Akapiga kelele, akisema, “Yesu Mwana wa Daudi, unirehemu.” Basi wale waliotangulia wakamkemea ili anyamaze; lakini yeye alizidi sana kupaza sauti, “Ee Mwana wa Daudi, unirehemu”. Yesu akasimama, akaamuru aletwe kwake; na alipomkaribia, alimwuliza, “Wataka nikufanyie nini?” Akasema, “Bwana, nipate kuona.” Yesu akamwambia, “Upewe kuona; imani yako imekuponya.” Mara hiyo akapata kuona, akamfuata, huku akimtukuza Mungu. Na watu wote walipoona hayo walimsifu Mungu.
TAFAKARI
JIFAHAMU NA UPIGE HATUA SAWA: Kipofu huyu alizoea kuomba sadaka kando ya njia. Kristo alipokuwa anapita na akaambiwa tu ni yeye, alidhihirisha kuwa alikuwa na macho ya imani akisema, “Yesu mwana wa Daudi unionee huruma.” Hakumwomba Kristo sadaka bali alipoulizwa na Kristo wataka nikufanyie nini? Akajibu “Bwana nipate kuona”. Yesu akamwambia upewe kuona. Huyu kipofu amedhihirisha kujifahamu na kuifahamu imani na kuomba lililo sahihi. Wewe leo hii Kristo anakuuliza wataka nikufanyie nini? Sehemu ya somo la kwanza kutoka katika kitabu cha Ufunuo inamkumbusha kila Mkristo kuwa umesahau upendo wa kwanza; rejea furaha uliyokuwa nayo wakati ulipokea sakramenti kwa mara ya kwanza au ukamwekea Mungu ahadi yoyote kwa mara ya kwanza. Unayo bado furaha na upendo huo, na kama haupo chukua hatua. Neno la Mungu limetuambia kumbuka ulikoanguka; tubu, fanya kwa furaha na kujituma kama ilivyokuwa kwanza.
SALA: Ee Bwana uniwezeshe kuitunza neema niliyoipokea kwa sakramenti ya ubatizo. Amina.